Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Watenda uhalifu mkubwa hawatokwepa mkono wa sheria, asema mwendesha mashtaka wa ICC akiwa Kenya

Watenda uhalifu mkubwa hawatokwepa mkono wa sheria, asema mwendesha mashtaka wa ICC akiwa Kenya

Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu, ICC, Fatou Bensouda, amesema hakuna mtu yeyote ambaye atatekeleza uhalifu mkubwa na kukwepa mkono wa sheria. Bi Bensouda amesema hayo katika mkutano na waandishi wa habari mjini Nairobi, Kenya.

Mapema wiki hii, amefanya mikutano na Rais Mwai Kibaki na Waziri Mkuu, Raila Odinga, na kuwasilisha masikitiko ya afisi yake kuhusu kuchelewa kwa serikali ya Kenya kuitikia baadhi ya maombi ya afisi hiyo kuhusu uchunguzi inaofanya.

Katika awamu ya kwanza ya safari yake nchini Kenya, Bi Bensouda amefanya pia mikutano na maafisa wengine wa ngazi ya juu wa serikali, na kusisitiza kuwa hakuna muda wa kupoteza katika kutimiza maombi ya afisi yake kwa serikali ya Kenya, kuhusu kesi inayowahusu wanasiasa wa Kenya na mtangazaji wa redio.

Ameelezea pia hofu yake kuhusu vitisho kwa mashahidi na kuongezeka mazingira ya hofu dhidi ya wale wanaodhaniwa kuwa washahidi wa ICC, familia zao na wale wanaohusishwa na ICC. Amesema vitisho dhidi ya mashahidi havikubaliki, na ni hatia, na kwamba serikali ya Kenya ina wajibu wa kuchunguza na kukabiliana na wanaofanya hivyo kisheria. Bi Bensouda amekutana na baadhi ya waathiriwa wa machafuko ya baada ya uchaguzi wa mwaka 2007 mjini Nakuru, na ataendelea kukutana na wengine kesho mjini Eldoret.