Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNESCO yalaani mauaji ya mpiga picha wa televisheni Syria

UNESCO yalaani mauaji ya mpiga picha wa televisheni Syria

Mkurugenzi Mkuu wa shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa, UNESCO Irina Bokova amelaani vikali mauaji ya mpiga picha wa televisheni wa Syria yaliyofanyika kwenye mji wa mashariki wa Deir Al-Zour nchini humo.

Katika taarifa yake, Mkuu huyo wa UNESCO, shirika lenye wajibu wa kulinda uhuru wa vyombo vya habari, pia ametaka kuachiwa huru mara moja kwa waandishi wa habari walioripotiwa kutekwa nyara.

Bokova amesema waandishi wa habari wanapaswa kuachiwa wafanye kazi yao kwa weledi na amerejelea tena wito wake kwa pande zote zinazozozana nchini Syria kuheshim haki za kiraia za waandishi wa habari na watumishi wa vyombo vya habari.

Mpiga picha huyo wa televisheni ya Syria Mohammed Al-Ashram aliuawa kwa kupigwa risasi tarehe 10 mwezi hu wakati akipiga picha tukio la mapigano kati ya majeshi ya serikali na vikosi vya upinzani na kifo chake kwa mujibu wa UNESCO kimefanya idadi ya watumishi wa vyombo vya habari waliouawa nchini Syria mwaka huu pekee kufikia 32.

.