Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kanuni za uwekezaji wenye kuwajibika katika kilimo kubuniwa: FAO

Kanuni za uwekezaji wenye kuwajibika katika kilimo kubuniwa: FAO

Shirika la chakula na kilimo, FAO, limetangaza kuidhinishwa kwa mkakati wa miaka miwili wa kubuni kanuni za uwekezaji wenye kuwajibika, kuheshimu haki za binadamu, riziki za watu na rasilmali. Mkakati huo umeidhinishwa na Kamati ya FAO kuhusu usalama wa chakula, CFS, mwishoni mwa kikao chake cha 39 kwenye makao makuu ya FAO mjini Roma.

Chini ya uongozi wa kamati ya CFS, mawaidha yatakusanywa kwenye ngazi za kimataifa na kikanda, ili kubuni sera zitakazohakikisha usalama wa chakula na lishe kwa wote. Kamati hiyo ya kimataifa itayahusisha mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa, mashirika ya umma, sekta ya kibinafsi, taasisi za utafiti wa kilimo, taasisi za kifedha na wakf za wafadhili wa kibinadamu.

Kanuni hizo zitaongozwa na sera zilizopo tayari. Shirika la FAO linakadiria kuwa uwekezaji unaohitajika kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa kilimo katika nchi zinazoendelea ili kufikia malengo ya mahitaji ifikapo mwaka 2050, ni dola bilioni 83 kila mwaka.