Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Brahimi akutana na Rais Assad na kurejelea wito wa kusitisha mapigano wiki hii

Brahimi akutana na Rais Assad na kurejelea wito wa kusitisha mapigano wiki hii

Mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa na Jumuiya ya nchi za Kiarabu kuhusu Syria, Lakhdar Brahimi, amekutana na kufanya mazungumzo na Rais Bashar al-Assad wa Syria kuhusu hali ilivyo nchini humo, na masuala yote yanayohusiana na mzozo wa Syria.

Bwana Brahimi amewaambia waandishi wa habari mjini Damascus kuwa mkutano wake na Rais Assad uliangazia pia hali ya siku zijazo, na matumaini kuwa hali iliyoko sasa itahitimishwa kwa kupata suluhu kwa mzozo wa Syria na kurejesha amani na utangamano nchini humo.

Mkutano na Rais Assad umefanyika katika awamu ya mwisho ya ziara yake katika nchi za Mashariki ya Kati, ambako tayari amekutana na viongozi katika nchi za Misri, Lebanon, Iran na Iraq.

Bwana Brahimi pia amerejelea wito wake kwa pande zote zinazozozana kusitisha mapigano wiki hii wakati Waislamu wakijiandaa kusherehekea siku kuu ya Eid al-Adha.

Nimezungumza na kila niliyekutana naye ndani na nje ya Syria kuhusu jukumu hili binafsi, ambalo si sehemu ya mpango wa amani tunaoitakia nchi hii. Ni jitihada zangu binafsi, na wito kwa kila mwanamume na kila mwanamke nchini Syria, wawe watu binafsi mitaani au vijijini au watu wenye silaha katika jeshi au upinzani. Ni wito kwa wote kusitisha mapigano kila mtu binafsi, na ikiwa kila mtu atafanya uamuzi binafsi, utakuwa uamuzi wa pamoja.