Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban ashangazwa na mapigano yalosababisha zaidi ya vifo 20 Libya

Ban ashangazwa na mapigano yalosababisha zaidi ya vifo 20 Libya

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban ki-Moon, ameelezea kushangazwa na mapigano katika mji wa Ban Walid nchini Libya, na hususan ripoti za mauji ya raia wengi kutokana na urushaji makombora kiholela. Bwana Ban amezikumbusha pande zote katika mapigano hayo kuhusu wajibu wao chini ya sheria ya kibinadamu ya kimataifa, na kutoa wito kwa serikali ya Libya na wale walio kwenye mji wa Ban Walid kuanza mara moja harakati za kuumaliza mzozo huo kwa njia ya amani.

Bwana Ban amesema anaamini kwamba serikali ya Libya ni lazima iwe na uwezo wa kupanua mamlaka yake na huduma zake ili kufikia kila eneo lililoko ndani ya mipaka yake. Ameongeza kuwa watu wa Libya waliweka imani yao katika serikali waliyoichagua mnamo mwezi Julai, na kutoa wito kwa raia wote kuungana ili waimarishe uwezo wa taasisi za kitaifa kote nchini.

Katibu Mkuu amesema kuwa wote wanaohusika katika mapigano hayo wanafaa kufahamu kuwa jamii ya kimataifa inafuatilia kwa karibu hali ilivyo, na kuongeza kuwa anaamini hali hiyo inaweza kutatuliwa kwa njia ya amani.