Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ulimwengu una chakula cha kutosha kumlisha kila mtu: Ban

Ulimwengu una chakula cha kutosha kumlisha kila mtu: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, amesema ulimwengu una chakula cha kutosha kuweza kumlisha kila mtu, na kutoa wito hatua zichukuliwe za kutokomeza njaa. Bwana Ban amesema hayo kwenye hafla ya kutoa tuzo ya kimataifa ya chakula, ambayo imefanyika mjini Des Moines, Iowa.

Katibu Mkuu amesema kutokomeza njaa kunahitaji uongozi bora wa kimataifa, na kwamba watu walio na njaa duniani wanahitaji viongozi wa kisiasa ambao wanafanya kupata chakula na lishe suala la kipaumbele.

Bwana Ban amesema hayo wakati zaidi ya wawakilishi elfu moja wa serikali, mashirika ya umma, sekta ya kibinafsi na wanasayansi wanakutana mjini Roma kuendelea kuimarisha kamati inayohusiana na usalama wa chakula kote duniani, ili iweze kutekelza jukumu lake muhimu.

Katika ulimwengu ulio na chakula kingi, hamna mtu yeyote anayestahili kuwa na njaa. Hamna mtoto anayestahili kuwa na afya mbovu kwa sababu ya utapia mlo. Hamna motto anayetakiwa kunyimwa nafasi ya kuwa na maisha mazuri hata kabla hajazaliwa kwa sababu mamake hakupata lishe ya kutosha akiwa na mamba. Kutokomeza njaa na utapia mlo kinaweza kutendeka. Ni kitu kizuri cha kufanya, cha busara na muhimu pia. Hatuna budi kulifanya hilo. Ulimwengu una chakula cha kutosha kumlisha kila mwanamke, mwanamume na kila mtoto.