Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Syria yaweza tumbukia katika mgogoro wa chuki baina ya makundi: Pillay

Syria yaweza tumbukia katika mgogoro wa chuki baina ya makundi: Pillay

Syria inaweza kutumbukia katika mgogoro wa chuki baina ya makundi yenye misimamo tofauti wakati huu ambapo jumuiya ya kimataifa imegawanyika juu ya hatua za kuchukua kumaliza mzozo huo uliodumu kwa miezi mwaka mmoja na nusu sasa.

Hiyo ni kauli ya Mkuu wa Tume ya Haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa, Navi Pillay aliyotoa leo mjini Geneva, Uswisi alipozungumza na waandishi wa habari.

Amesema kile kilichotokea Bosnia bado kinakumbukwa na hivyo kinapaswa kuwa onyo kwa jumuiya ya kimataifa kwa kuwa kimya kwenye mgogoro wa Syria.

Bi. Pillay amesema kitendo cha majeshi ya serikali kutumia silaha nzito bila kushambulia popote na kuharibu miji na kile cha wapinzani kutumia mabomu na kuua na kujeruhi raia hakiwezi kusamehewa na vitendo hivyo vinaweza kusababisha uhalifu wa kivita au uhalif dhidi ya binadamu.

"Maelfu ya wanaume, wanawake na watoto tayari wameuawa, wamejeruhiwa, wameteswa na kulazimika kuhama makwao. Kwa kuendelea kugawanyika, jamii ya kimataifa inawezesha kuendelea kwa mateso haya, na kuweka mazingira ya mzozo mkubwa zaidi wa kikanda. Kadri mzozo huu mbaya unavyoendelea, ndivyo unavyokuwa hatari zaidi si tu kwa siku zijazo za Syria, bali pia kwa kanda nzima. Tayari mzozo kuvuka mpaka wa Uturuki unahatarisha amani na usalama wa kikanda. Nahofia watoto wa Syria, wengi wao ambao wataachwa na makovu ya uchungu na mateso wanayopitia. Hamna mtoto anayestahili kupitia wanayopitia hawa watoto, na hasa ukatili huu ukitendwa na serikali yao, jeshi lao au jirani zao wenyewe".