Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kila mmoja anaweza kudhibiti uhalifu unaopangwa: UM

Kila mmoja anaweza kudhibiti uhalifu unaopangwa: UM

Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayohusika na udhibiti wa madawa ya kulevya na uhalifu, UNODC imezungumzia vitendo vya uhalifu unaopangwa ikiwemo usafirishaji wa madawa ya kulevya, na kutaka nchi zote duniani kuwa makini na kuchukua hatua za mapema za kubadilishana taarifa juu ya kupambana na vitendo hivyo.

Riikka Puttonen ambaye ni afisa kutoka kitengo cha uhalifu unaopangwa katika ofisi hiyo amesema vitendo kama vile ukataji haramu wa magogo, usafirishaji wa binadamu na madawa ya kulevya vinatishia maendeleo, ulinzi na utawala wa kisheria.

Amesema wakati vitendo vya uhalifu unaopangwa baina ya raia wa nchi mbali mbali duniani ukigharimu dola Bilioni 870, madhara wanayopata waathirika wa vitendo hivyo hayapimiki.

Hata hivyo amesema kila mtu ana uwezo wa kuzuia vitendo vya uhalifu uliopangwa mathalani kwa kutonunua bidhaa bandia kama vile DVD zinazotengenezwa kinyume cha sheria.

“Uhalifu unaopangwa uko kila pahali. Tunauona kila pahali lakini mara nyingi tunakuwa hatutambui. Na ndiyo maana tunapaswa kuwa na misingi ya uamuzi kama walaji wa nini cha kununua na jinsi ya kutumia.”