Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban alaani mashambulio nchini Syria, ataka pande husika zijadiliane

Ban alaani mashambulio nchini Syria, ataka pande husika zijadiliane

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon amelaani vikali mashambulio ya kigaidi yaliyofanyika kwa wakati mmoja katika mji mkuu wa Syria, Damascus, yaliyosababisha vifo na majeruhi kadhaa na amerejelea msimamo wake wa kuzisihi pande zote husika kuingia katika meza ya majadiliano ili kupatia suluhu ya kisiasa ya mzozo huo.

Taarifa iliyotolewa na msemaji wa Ban, imemkariri Katibu Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa akisema kuwa mgogoro wa Syria unaweka msingi wa mashambulio ya kigaidi na vitendo vya kihalifu ambapo imeelezwa kuwa mmoja wa washambuliaji alikuwa anaendesha gari la wagonjwa lililokuwa limesheheni mabomu.

Ban pia ameeleza wasiwasi wake juu ya hatma ya watu wanaoshikiliwa mateka katika kambi ya jeshi la anga la Syria, huko Harasta, kaskazini mashariki mwa Damascus ambapo mashambulio hayo yalifanyika jumatatu usiku.

Zaidi ya watu 20,000 wengi wao wakiwa raia wamekufa nchini Syria tangu kuanza kwa harakati dhidi ya Rais Bashar al-Assad wa nchi hiyo mwaka jana ambapo kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa raia Milioni Mbili na Nusu wa nchi hiyo wanahitaji msaada wa dharura wa kibinadamu.