Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Serikali zinatakiwa kuwasikiliza watu: Ban

Serikali zinatakiwa kuwasikiliza watu: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, ametoa wito kwa serikali kote duniani ziwasikilize raia, wakati wa hotuba yake kwenye kongamano la kimataifa kuhusu demokrasia, ambalo linaendelea mjini Strasbourg, Ufaransa.

Kongamano hilo linalomalizika tarehe 11 Oktoba, limewaleta pamoja wataalam wa marekebisho na viongozi wa kimataifa ili kutambua jinsi ya kuitikia changamoto zinazoukabili ulimwengu kwa sasa kiuchumi, kijamii na kisiasa, kwa njia ya demokrasia, na kuyafikia matakwa ya watu, kulingana na maadili na tamaduni zao.

Bwana Ban amesema changamoto moja kuu inayoukabili ulimwengu kwa sasa ni desturi ya kuwasikiliza watu. Amesema Umoja wa Mataifa unachukua hatua za kina ili kuendeleza demokrasia kote duniani. Ameongeza kuwa kila serikali zinaposhindwa kutekeleza wajibu wao kulingana na sheria za kimataifa, ni lazima zikumbushwe kuhusu majukumu zilizo nayo.