Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban aonya uwezekano wa mgogoro wa Syria kusambaa maeneo mengine

Ban aonya uwezekano wa mgogoro wa Syria kusambaa maeneo mengine

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-Moon ameonya uwezekano wa mgogoro wa Syria kusambaa katika maeneo jirani kutokana na ongezeko la wasiwasi wa hali ya usalama katika mpaka wa nchi hiyo na Uturuki.

Onyo hilo la Ban linafuatia shambulio la makombora kutoka Syria siku ya Jumatano dhidi ya mji mmoja nchini Uturuki, lililofuatiwa na Uturuki kujibu mashambulizi.

Kutokana na hali hiyo, Msemaji wa Umoja wa Mataifa Martin Nesirky amemnukuu Katibu mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa akizitaka pande zote husika kuacha matumizi ya nguvu na badala yake zijizuie na zijitahidi kutafuta suluhisho la kisiasa katika mvutano huo.

"Katibu Mkuu ana hofu na ongezeko la mvutano katika mpaka wa Syria na Uturuki, na kila wakati ameonyesha wasiwasi wake juu ya uwezekano wa mgogoro huo wa Syria kuenea nchi jirani kama ilivyo kwa Uturuki. Kadri hali ya amani inavyozidi kuwa mbaya nchini Syria ikiwemo mashambulizi ya wiki hii ya kigaidi huko Aleppo yaliyosababisha vifo vya makumi ya watu ikiwemo raia, uwezekano wa kuwepo kwa mgogoro wa kikanda na hata vitisho kwa amani na usalama duniani vinaongezeka.