Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Umoja wa Afrika uendelee kupinga mapinduzi ya kijeshi: Skelemani

Umoja wa Afrika uendelee kupinga mapinduzi ya kijeshi: Skelemani

Serikali ya Botswana imeutaka Umoja wa Afrika kuendelea na msimamo wake wa kupinga mapinduzi ya kijeshi yanayoondoa serikali madarakani kinyume cha katiba.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Botswana Phandu Skelemani akihutubia Jumatatu ambayo ni siku ya mwisho ya mjadala wa wazi wa mkutano wa 67 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani ametaja mapinduzi ya kijeshi yaliyofanyika huko Mali na Guinea mapema mwaka huu na kusema yamekumbusha enzi za kusikitisha za siasa za kibinafsi barani Afrika.

"Matukio haya yanadidimiza maendeleo yaliyofanywa na Afrika hadi leo ya kulinda na kuendeleza demokrasia, utawala bora, heshima kwa haki za binadamu na utawala wa sheria. Hivyo basi tunautaka Umoja wa Afrika uendelee kushikilia msimamo wake wa kukataa mabadiliko ya serikali kinyume cha katiba na tunaiomba Jumuiya ya kimataifa iunge mkono Umoja wa Afrika katika suala hili.”

Katika hatua nyingine Skelemani amesema pamoja na nchi yake kuunga mkono makubaliano ya hivi karibuni kati ya Sudan na Sudan Kusini, ya kumaliza tofauti zao, bado ina wasiwasi kuhusu hali ya wasiwasi wa usalama kati ya nchi mbili hizo.