Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Eneo la Sahel limo katika hali tete:Ban

Eneo la Sahel limo katika hali tete:Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, ameuambia mkutano wa ngazi ya juu kuhusu eneo la Sahel kuwa hali katika eneo hilo sasa ni tete. Amesema misukosuko ya kisiasa, hali mbaya ya hewa pamoja na hali duni ya kiuchumi vinachangia hali ya hatari kaatika eneo hilo.

Amesema watu na serikali za eneo hilo zinahitaji usaidizi wa dharura wa kimataifa. Ameongeza kuwa hakuna suluhisho rahisi, na kwamba chanzo cha hali hii kinazidi uwezo wa mataifa binafsi kukabiliana nacho, na hivyo, kunahitajika hatua za pamoja za kikanda.

Ametangaza kuwa kufuatia ombi la Baraza la Usalama, Umoja wa Mataifa unaandaa mkakati wa pamoja wa kikanda kuhusu eneo la Sahel, ambao utakabiliana na hali duni ya usalama, kuzuia na kukabiliana na mizozo mikubwa, na kuendeleza uongozi wa kidemokrasia na heshima ya haki za binadam, pamoja na kukabiliana na tishio la ugaidi, kuendeleza ushirikishaji wa wote, maridhiano na upatanishi.