Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kusuluhisha matatizo sugu duniani kunahitaji mchango wa sawa wa wanawake:UM

Kusuluhisha matatizo sugu duniani kunahitaji mchango wa sawa wa wanawake:UM

Mkuu wa kitengo cha wanawake cha UNWomen katika Umoja wa Mataifa, Michelle Bachelet, amesema kuwa ulimwengu unatambua kuwa kutafuta suluhu kwa matatizo sugu zaidi duniani kunahitaji mchango wa wanawake kikamilifu na kwa usawa. Katika mkutano wa ngazi ya juu kuhusu kuimarisha haki kwa wanawake, Bi Bachelet amesema kuwa utambuzi huu ni lazima uende sambamba na vitendo.

Amesema hatua zinahitajika kwa sababu uongozi wa kisheria mara kwa mara huwaacha nje wanawake. Ameongeza kuwa takwimu zinaonyesha kuwa kila wanawake 8 kati ya 10 hawapati huduma za mfumo wa haki katika nchi zao. Amesema mfumo wa uongozi wa kisheria unahitaji kuwahakikishia wanawake usawa wa haki, nafasi na kuhusishwa, na kuongeza kuwa haki na usawa ndiyo misingi ya jamii bora, uchumi imara na demokrasia.

Amekaribisha ahadi zilizowekwa na mataifa mengi za kutekeleza sheria za kutokomeza dhuluma na ubaguzi dhidi ya wanawake, na kuendeleza usawa katika kufanya uamuzi muhimu. Amesema wanawake kote ulimwenguni wamechoka kusubiri haki, na kwamba wanahitaji hatua kuchukuliwa sasa, kwani kutochukuwa hatua kunaruhusu uhalifu dhidi ya wanawake kuendelea.