Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ushirikiano wa mpango wa lishe bora walenga watu milioni 15 Afghanistan

Ushirikiano wa mpango wa lishe bora walenga watu milioni 15 Afghanistan

Wizara ya Afya ya Afghanistan, ikishirikiana na Wakfu wa Khalifa Bin Zayed Al Nahyan, Shirikisho la kimataifa la lishe bora (GAIN) na shirika la mpango wa chakula la Umoja wa Mataifa, (WFP), leo imezindua ushirikiano ambao utawawezesha watu milioni 15 raia wa Afghanistan kupata chakula chenye lishe bora, ikiwemo ngano na mafuta ya kupikia.

Ushirikiano huo unalenga kupunguza viwango vya ukosefu wa vitamini na madini mengine miongoni mwa watu, na hasa watoto na wanawake wenye umri wa uzazi, kupitia mradi unaounga mkono mpango wa serikali wa kukabiliana na lishe duni.

Mradi huo utazihusisha viwanda vikubwa vya kutengeneza mafuta ya kupikia na unga wa ngano, huku vifaa vya kuongeza virutubishaji vyenye lishe na mafunzo ya kitaaluma yakitolewa kwa viwanda hivyo.