Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Juhudi zaidi zahitajika kudhibiti usambazaji wa silaha ndogondogo: Ban

Juhudi zaidi zahitajika kudhibiti usambazaji wa silaha ndogondogo: Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki-Moon, ametoa wito kwa serikali kote duniani kufanya juhudi zaidi ili kukomesha usambazaji wa silaha ndogondogo haramu. Katika ujumbe ulowasilishwa na naibu Katibu Mkuu, Jan Eliasson, Bwana Ban amesema kuwa silaha ndogondogo haramu zinabaki kupendelewa na wale wanaotaka kuasi uongozi wa kisheria, kueneza hofu na kuzorotesha usalama, pamoja na kuyafikia malengo ya kihalifu.

Ujumbe huo umetolewa wakati wa mkutano wa pili wa kukagua mpango kuchukua hatua kuhusu silaha ndogondogo unaofanyika kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York.

Bwana Ban amesema kuwa gharama ya matumizi ya silaha ndogondogo kwa binadamu, hasa katika vita vya silaha, uharamia, magenge na ghasia zingine za uhalifu ni dhahiri, na kwamba zaidi ya watu nusu milioni huuawa kila mwaka kutumia silaha ndogondogo. Amesema wengi wa hawa wanaoathirika, huwa ni raia, na hasa walo maskini zaidi.