Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WHO yasema hospitali na vituo vya afya vimeharibiwa kwa viwango vikubwa nchini Syria

WHO yasema hospitali na vituo vya afya vimeharibiwa kwa viwango vikubwa nchini Syria

Shirika la Afya Duniani, WHO, limesema wizara ya Afya nchini Syria inakadiria kuwa hospitali 38 na vituo vingine 149 vya afya vimeharibiwa kwa kiasi kikubwa, au hata kabisa, na hivyo kufanya utoaji wa huduma za afya kuwa mgumu.

Mkurugenzi wa Kudhibiti Matukio ya Dharura na Hatari katika, WHO, Richards Brennman, amesema shirika hilo linahusika kwa kiwango kikubwa na masuala ya kibinadamu nchini Syria kwa sasa, na kila mmoja anatambua mazingira yalivyo magumu kwa mashirika ya kutoa huduma za kibinadamu nhcini humo.

Amesema changamoto kubwa zaidi kwa sasa ni uwezo wa kufikisha huduma za matibabu kwa wagonjwa na hata wahudumu wa kibinadamu walioko nchini Syria. Amesema, mbali na kuwepo uwezo mdogo wa watu kufikia huduma za afya, kuna uhaba wa madawa na usalama mdogo kwa watoaji huduma za afya na vituo vya afya vyenyewe. Shirika la WHO limesema, kwa hivi sasa linatumia mashirika yasiyo ya kiserikali ya wenyeji nchini Syria kutoa huduma za afya.