Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM waunga mkono Chanjo ya Magonjwa ya Kupooza na Surua nchini Afghanistan

UM waunga mkono Chanjo ya Magonjwa ya Kupooza na Surua nchini Afghanistan

Zaidi ya wahudumu wa afya 27,000 na watu wanaojitolea wametawanyika kwenye mikoa 16 nchini Afghanistan kwa muda wa majuma mawili yaliyopita kwa lengo la kuangamiza ugonjwa wa kupooza kupitia kwa kampeni mpya ya Umoja wa Mataifa. Kampeni hiyo inayotekelezwa na wizara ya afya ya umma nchini Afghanistan, mapema juma hili ilitoa chanjo kwa zaidi ya watoto milioni 5.6 walio na umri wa kati ya miezi tisa na miaka kumi.

Taufiq Mashal ambaye ni mkurugenzi wa madawa kwenye wizara anasema kuwa awamu hii ya kwanza inajumuisha chanjo dhidi ya magonjwa ya kupooza na surua. Ameongeza kuwa awamu ya pili inatarajiwa kung’oa nanga mwezi Septemba na itaendeshwa kwenye mikoa 18 iliyosalia nchini Afghanistan.