Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kundi la Kuchukua Hatua ya Mzozo wa Syria kukutana Geneva katika ngazi ya mawaziri

Kundi la Kuchukua Hatua ya Mzozo wa Syria kukutana Geneva katika ngazi ya mawaziri

Mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa na Umoja wa nchi za Kiarabu Kofi Annan ametangaza Jumatano kwamba kutakuwa na mkutano maalumu wa kundi la kuchukua hatua kuhusu masuala ya Syria mjini Geneva hapo June 30. Mwaliko umetumwa kwa mawaziri wa wajumbe watano wa kudumu wa Baraza la Usalama pamoja na nchi zingine wanachama wanaohusika.

Lengo la mkutano huo amesema bwana Annan ni kutafuta njia ya utekelezaji kamili wa mpango wa vipengee sita vya  wa amani ambao unajumuisha usitishaji mapigano mara moja na kufikia makubaliano ya muongozo wa kipindi cha mpito cha kisiasa katika taifa hilo la Mashariki ya Kati kwa manufaa ya watu wa Syria. Bwana Annan amesema anatarajia kuwa na mkutano utakaozaa matunda na anatumai muafaka utafikiwa kuhusu hatua za kumaliza ghasia na kuleta amani kwa watu wa Syria ambao kwa sasa wanateseka sana.

(SAUTI YA KOFI ANNAN)

Mwaliko umepelekwa pia kwa Umoja wa Mataifa, Umoja wa nchi za Kiarabu, Muungano wa Ulaya. Iraq, Kuwait na Qatar. Iran haijaalikwa ingawa mwakilishi maalum awali alielezea nia ya kuona Iran inashiriki juhudi za amani ya Syria.