Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uongozi Thabiti na Mpango wa Kina wahitajika kwa ajili ya eneo la Sahel:Amos

Uongozi Thabiti na Mpango wa Kina wahitajika kwa ajili ya eneo la Sahel:Amos

Mratibu Mkuu wa Maswala ya Kibinadamu katika Umoja wa Mataifa, Bi Valerie Amos, amesema, ili kuizuia hatari ya njaa katika eneo la Sahel kupea na kugeuka kuwa janga, uongozi thabiti na mpango wa kina unahitajika ili kuliitikia swala la mahitaji ya eneo hilo. Bi Amos amekuwa akiyazuru mataifa ya Burkina Faso na Senegal kwenye maeneo yaloathiriwa na ukame magharibi mwa mataifa hayo.

Akikamilisha ziara yake hiyo ya siku nne, Bi Amos amesema kuwa hatua za haraka na zenye utaratibu mzuri, pamoja na ukarimu wa mataifa jirani na jamii ya kimataifa vitahitajika ili kuzuia janga la njaa katika eneo hilo, ambako watu milioni 15 wanakabiliwa na uhaba wa chakula. Watu milioni 2.8 katika taifa la Burkina Faso wanakabiliwa na tatizo la njaa, huku watu laki nane wakikabiliwa na tatizo hilo nchini Senegal. Mataifa mengine yenye kukabiliwa na tatizo la njaa kwenye eneo la Sahel ni Chad, Mali, Mauritania, na Niger, pamoja na maeneo ya kaskazini mwa Cameroon na Nigeria.