Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Balozi Mahiga Asikitishwa na kuuawa kwa Mwandishi Habari Somalia

Balozi Mahiga Asikitishwa na kuuawa kwa Mwandishi Habari Somalia

Mjumbe maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia Augustine Mahiga, amesikitishwa na habari za kuuawa kwa mwandishi habari leo mjini Mogadishu. Mwandishi huyo habari wa Radio Shabelle, Ahmed Addow Anshuur, amepigwa risasi na kuuawa Alhamis asubuhi mjini Mogadishu. Yeye ndiye mwandishi wa habari wa 6 kuuawa nchini Somalia mwaka huu.

Balozi Mahiga amesema kuwa, ingawa inajulikana wazi kuwa waandishi wa habari nchini Somalia ndio wanaofanya kazi katika mazingira mabaya zaidi kote duniani, hiyo haiwezi kuwa sababu ya kukubali kwa urahisi mauaji ya mtu yeyote.

Kwa mujibu wa Kamati ya Kulinda haki za waandishi wa habari, CPJ, Somalia imekuwa nchi ya pili hatari zaidi kwa uandishi habari mwaka 2012, baada ya Syria.

Balozi Mahiga ameongeza kuwa mauaji ya leo yanasikitisha zaidi, hasa ukizingatia kuwa yanatokea mara tu baada ya kongamano la kikatiba kuhusu haki ya kujieleza, ambako viongozi wa Somalia waliapa kuunga mkono uhuru wa uandishi habari.

Balozi Mahiga ametoa wito kwa serikali ifanye uchunguzi na kuhakikisha kuwa wahusika wanachukuliwa hatua za kisheria, na kusema kwamba vitendo vihyo vya kikatili ni lazima vikomeshwe.