Ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme kwa ufadhili wa UM waanza Sierra Leone
Ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme kwa usaidizi wa Umoja wa Mataifa kaskazini Magharibi mwa Sierra Leone kwa lengo la kuwapa wenyeji wa eneo hilo kawi umeng’oa nanga.
Kituo hicho kinachojengwa kwenye mto Bankasoka karibu na mji wa Port Loko kinafadhiliwa na serikali ya China na shirika la maendeleo la Umoja wa Mataifa UNIDO.
Mkurugenzi mkuu wa UNIDO Kandeh Yumkella aliyeandamana na rais wa Sierra Leone Ernest Bai Koroma wakati wa uzinduzi wa mradi huo amesema kuwa vituo kama hivyo kwenye sehemu za vijijini nchini Sierra Leone vitachangia katika kuimarika kwa miradi ya kilimo kupitia unyunyizaji wa maji.