Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Hatima ya Thomas Lubanga kujulikana jumatano machi14

Hatima ya Thomas Lubanga kujulikana jumatano machi14

Uamuzi wa ama kuwa na hatia au kutokutwa na hatia dhidi ya kesi ya mpiganaji wa zamani kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Thomas Lubanga Dyilo kutolewa Jumatano na majaji wa mahakama ya kimataifa ya uhalifu ICC.

Mahakama hiyo itatoa uamuzi kwa kuzingatia misingi ya mkataba wa Roma mapema asubuhi mjini Hague katika hukumu itakayotolewa hadharani.

Kesi dhidi ya Thomas Lubanga ni ya kwanza kutolewa hukumu na mahakama ya ICC na ilianza Januari 26 mwaka 2009 na maelezo ya mwisho kuhusu kesi hiyo zimetolewa Agosti 25 na 26 mwaka 2011.

Kwa mujibu wa mkataba wa Roma ili mahakama imkute na hatia mshitakiwa mahakama lazima ishawishike kwamba hatia dhidi ya mshitakiwa iko bayana bila shaka yoyote.

Endapo atakutwa na hatia mahakama itaamua baadaye kifungo muafaka dhidi ya mshitakiwa.

Na endapo mshitakiwa hatokutwa na hatia basi mahaka pia itapaswa kuzingatia misingi ya mkataba wa Roma kuhusu hatua itakayofuata.

Hadi sasa kesi 14 zimefikishwa kwenye mahakama ya ICC na nne kati ya hizo zinasikilizwa mahakamani.

 Kwa jumla 7 ziko katika uchunguzi nchini Uganda, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Darfur Sudan, Kenya, Libya na Ivory Coast.