Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Walinda amani wawili wanaohudumu kwenye kikosi cha UNAMID wajeruhiwa

Walinda amani wawili wanaohudumu kwenye kikosi cha UNAMID wajeruhiwa

Walinda amani wawili wanaohudumu kwenye kikosi cha pamoja cha Muungano wa Afrika na Umoja wa Mataifa cha kulinda amani kwenye jimbo la Darfur nchini Sudan UNAMID walijeruhiwa wakati watu waliokuwa wamejihami walipofyatulia risasi basi walilokuwa wakisafiria karibu na mji wa El Dein ulio magharibi mwa Sudan.

Wawili hao walio kwenye kikosi cha polisi cha UNAMID walipata majeraha ya risasi kwenye tukio hilo lililotokea umbali wa kilomita moja kutoka kwa kituo chao. Jumla ya wanajeshi watano wa UNAMID wamejeruhiwa kwenye visa vya mashambulizi tangu mwanzo wa mwaka huu. Mapigano kati ya wanajeshi wa Sudan na waasi yamesababisha idadi kubwa ya watu kuhama mamkwao kwenye jimbo la Darfur tangu mwaka 2003.