Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

WTO inatetea mtazamo uliopitwa wakati wa usalama wa chakula:De Schutter

WTO inatetea mtazamo uliopitwa wakati wa usalama wa chakula:De Schutter

Mwakilishi maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu masuala ya haki ya chakula Oliver de Schutter amesema utandawazi unatoa washindi wakubwa na wapotezaji wakubwa. Lakini pale ambapo mifumo ya chakula inahusika kupoteza maana yake ni kutumbukia katika umaskini na njaa.

Amesema mtazamo wa usalama wa chakula ambao unazidisha mgawanyiko baina ya maeneo yenye akiba ya chakula na yenye upungufu, baina ya wasafirishaji na waingizaji na baina ya washindi na wanaoshindwa kwa kifupi hauwezi kukubalika.

De Schutter amesema athari za taratibu za biashara haziwezi kuangaliwa tena katika ngazi ya taifa pekee ni lazima ziwe makini na zizingatie nini hasa kinachosababisha usalama wa chakula, ziangalie nani anazalisha kwa ajili ya nani? Kwa gharama gani, chini ya masharti gani na kwa athari gani za kiuchumi, kijamii na kimazingira .

Amesisitiza kuwa haki ya chakula sio bidhaa na ni lazima watu waache kuichukulia kwa mtazamo huo. Amesema amezungumza na mkurugenzi wa shirika la kimataifa la biashara WTO na kusisitiza kuwa mijadala ya haki ya chakula lazima izingatie hatari ya nchi masikini kutegemea sana katika biashara.