Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Kamishna wa haki za binadamu ahofia maafa zaidi Syria

Kamishna wa haki za binadamu ahofia maafa zaidi Syria

Mambo imezidi kuchacha nchini Syria ambako ripoti zinasema kuwepo kwa ongezeko la watu wanaopoteza maisha, Kamishna wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa ameonya juu ya kile alichokiita uwezekano wa kusambaa machafuko katika maeneo ya miji mingine muhimu.

Duru zinasema kuwa tangu kuanza kwa wimbi la kudai mageuzi nchini Syria zaidi ya watu 5,000 wamepoteza maisha na wengine wakijeruhiwa kutokana na mashambulizi yanayoendeshwa na vikosi vya serikali dhidi ya waandamanaji.

Kamishna wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Bi Navy Pillay, amesema kuwa mbinyo mkali unaotekelezwa na vikosi vya serikali dhidi ya waandamanaji unatishia kuzusha machafuko mengine mapya katika miji kadhaa.

Bi Pillay ambaye hata hivyo hakuwa tayari kudhibitisha juu ya ripoti zinazosema kuwa vikosi vya serikali vimeendesha mashambulizi makubwa kwenye maeneo kadhaa, lakini hata hivyo amesema kuwa nguvu kubwa inayotumiwa na serikali ni ishara tosha kuwa mambo sasa yanazidi kuharibika.

Amesema duru kadhaa zimefahamisha juu ya hatua iliyochukuliwa na serikali ya kusambaza malori na magari mengine yakiwa na silaha kwa ajili ya kuwaandama wapiganaji.