Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mazingira ya kifo cha Gaddafi lazima yachunguzwe asema mwakilishi wa UM

Mazingira ya kifo cha Gaddafi lazima yachunguzwe asema mwakilishi wa UM

Kiongozi wa zamani wa Libya kanali Muammar Gaddafi na mwanaye wa kiume hawakutendewa vyema na wameuawa katika mazingira ya kutatanisha ambayo lazima yachunguzwe amesema afisa wa Umoja wa Mataifa.

Ian Martin, mwakilishi maalumu wa Katibu Mkuu nchini Libya ameliambia Baraza la Usalama leo Jumatano kwamba mauaji kama hayo mjini Sirte pia ni kinyume na maagizo ya baraza la mpito la Libya.

Ameongeza kuwa tukio hilo litachunguzwa pia na tume ya kimataifa itakayoandaliwa na baraza la haki za binadamu. Kabla ya hapo Martin alisema tangazo la ukombozi mjini Benghazi ni mwanzo mpya kwa watu wa Libya.