Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mwakilishi wa UM athamini maandalizi ya uchaguzi mkuu DR Congo

Mwakilishi wa UM athamini maandalizi ya uchaguzi mkuu DR Congo

Mkuu wa operesheni za kulinda amani za Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo amezuru mashariki mwa nchi hiyo katika mji wa Bukavu jimbo la Kivu ya Kusini kutathimini maandalizi ya uchaguzi mkuu ujao katika taifa hilo kubwa la Afrika.

Katika ziara yake ya siku mbili Roger Meece ambaye ni mwakilishi maalumu na mkuu wa mpango wa Umoja wa Mataifa wa MONUSCO amewahahakikishia maafisa wa serikali kwamba MONUSCO itaendelea kuwasaidia maandalizi kwa ajili ya uchaguzi wa Rais na wabunge uliopangwa kufanyika Novemba 28 mwaka huu.

Katib Mkuu wa tume ya taifa ya uchaguzi CENI bwana Eugene Birhenjira amemwambia Meece kwamba maandalizi yanakwenda vyema na vifaa vya uchaguzi vimeanza kuwasili kwa msaada wa kiufundi wa MONUSCO. Pia amesema watahakikisha uchaguzi unafanyika kwa amani na utulivu, na polisi 4000 wa ziada watapelekwa katika vituo vya kupigia kura .