Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Uharamia umepita mipaka na nia za kiuchumi:Ban

Uharamia umepita mipaka na nia za kiuchumi:Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema uharamia umevuka mipaka ya kitaifa na haja za kiuchumi. Akizungumza kwenye Baraza la Usalama ambalo leo limekutana kujadili uharamia katika ghuba ya Guinea, amesema uharamia huo una athari mbaya kwa biashara ya Afrika ya Magharibi na dunia nzima kwa ujumla hususani kwa washirika wakubwa wanaofanya biashara na Afrika Magharibi kama Marekani, Asia na Ulaya.

Ban amesema kumekuwa na visa vipya vya uharamia na unyang’anyi wa kutumia silaha katika vyombo vya usafiri wa majini kwenye mwambao wa Afrika ya Magharibi ambavyo vitakuwa na athari kubwa katika maendeleo ya chumi na usalama pia.

Ameongeza kuwa tishio ni kubwa kwa sababu eneo kubwa la Ghuba ya Guinea halina uwezo wa kuhakikisha kuna biashara salama ya majini, kuna uhuru wa kusafiri, kulinda maliasili ya majini na kuhakikisha usalama wa watu na mali zao.