Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Bila kukabiliana na hali ya jangwa umasikini hauwezi kumalizika:UM

Bila kukabiliana na hali ya jangwa umasikini hauwezi kumalizika:UM

Wakuu wa nchi wanaokutana kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa leo wamejadili utekelezaji wa mkataba wa Umoja wa Mataifa wa kupambana na hali ya jangwa hasa katika nchi zinazokabiliwa na ukame mkubwa hususani barani Afrika. Mkutano huu wa ngazi ya juu unaofanyika kwenye Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa una lengo la kuchagiza maendeleo endelevu na kutokomeza umasikini.

Akitoa ujumbe maalumu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema mara nyingi jumuiya ya kimataifa inachukua hatuua ikiwa imechelewa sana, akitoa mfano wa pembe ya Afrika Ban amesema zaidi ya watu milioni 13 nchini Djiboti, Ethiopia, Kenya na Somalia wanahitaji msaada wa haraka kutokana na ukame.

Lakini amesisitiza ukame sio lazima usababishe njaa, hatua zinahitaji kuchukuliwa haraka kudhibiti hali ya ukame na jangwa kabla havijaleta madhara makubwa na kuongeza kuwa endapo haitodhibitishwa mapema basi itarejesha nyuma juhudi za kufikia malengo ya maendeleo ya milenia. Lc Gnacadja ni katibu mkuu mtendaji wa mpango wa Umoja wa Mataifa wa kukabiliana na hali ya jangwa UNCCD.