Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Baraza la usalama la UM laongeza muda wa kikosi cha UM nchini Ivory Coast

Baraza la usalama la UM laongeza muda wa kikosi cha UM nchini Ivory Coast

Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa limeongeza muda wa kuhudumu kwa kikosi cha kulinda amani cha Umoja wa Mataifa nchini Ivory Coast (UNOCI) kwa mwaka mmoja zaidi ili kulisaidia taifa hilo kukabiliana na changamoto zinazolikabili kufuatia ghasia za uchaguzi mkuu uliopita.

Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa liliamua kuwa kikosi cha (UNOCI) kitasalia nchini Ivory Coast hadi tarehe 31 mwezi Julai mwaka 2012 na wanajeshi wake 9,800 wakiwemo wanajeshi 2000 waliopelekwa nchini humo mapema mwaka huu.

Taifa hilo la Afrika Magharibi linajaribu kujikwamua kutoka kwa mzozo uliomalizika mwezi Aprili wakati rais wa zamani Laurent Gbagbo alipojisalimisha na kumaliza miezi kadha ya machafuko baada ya kukataa kung’atuka madarakani aliposhindwa kwenye uchaguzi na mpinzani wake rais wa sasa Alassane Ouattara.