Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wafanyakazi wawili wa UNMIS kati ya sita waliokamatwa jana wameachiliwa Kadugli

Wafanyakazi wawili wa UNMIS kati ya sita waliokamatwa jana wameachiliwa Kadugli

Taarifa kutoka Sudan zinasema wafanyakazi wawili kati ya sita wa mpango wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan UNMIS waliokamatwa jana leo wameachiliwa kama anavyothibitisha msemaji wa UNMIS Kouider Zerrouk.

(SAUTI YA KOUIDER ZERROUK)

“Anasema tumearifiwa kwamba wafanyakazi wawili kati ya sita waliokamatwa jana uwanja wa ndege wa Kadugli wameachiliwa na kurejea ofisi za UNMIS Kadugli wakiwa salama . Tunakaribisha hatua hii ya jeshi la Sudan Kadugli hata hivyo tunatoa wito kwa pande zote na uongozi wa eneo hilo na hususani idara ya ujasusi ya jeshi kuwaachilia mara moja wengine wane ambao badio wanashikiliwa Kadugli.”

UNMIS imelaani vikali kukamatwa jana kwa wafanyakazi hao wa kitaifa ambao walikuwa wakisafiri kutoka uwanja wa ndege wa Kadugli kuelekea Wau kikazi.Watu hao wanadaiwa kukamatwa na  majasusi wa jeshi la Sudan na UNMIS inasema kwa mujibu wa mkataba kati ya Sudan na UNMIS , serikali ya nchi hiyo inapaswa kuwasilisha ushahidi kwa mwakilishi maalumu wa Katibu Mkuu kabla ya kuchukua hatua yoyote dhidi ya wafanyakazi wa UNMIS wa kitaifa na kimataifa na hivyo UNMIS imetaka wafanyakazi wake hao kuachiliwa mara moja.