Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Amos alaani Wapalestina kuondolewa kwa nguvu kwenye makazi yao

Amos alaani Wapalestina kuondolewa kwa nguvu kwenye makazi yao

Mratibu wa masuala ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa OCHA leo ametoa wito wa kusitisha vitendo vya kuwaondoa kwa nguvu Wapalestina kutoka Jerusalem na maeneo mengine ya Ukingo wa Magharibi akisema mipango ya Israel inaathari zisizokubalika kwa jamii ya Wapalestina.

Katika siku ya kwanza ya ziara yake ya siku nne kwenye himaya ya Palestina inayokaliwa na Israel Bi Valarie Amos amezuru Jerusalem Mashariki na kijiji cha Nabi Samwil kwenye Ukingo wa Magharibi.

Bi Amos ameona uzio pia ambao Israel inasema imejenga kwa sababu za usalama na kubaini kwamba asilimia 85 ya ya njia za uzio huo zipo ndani ya Ukingo wa Magharibi na matokeo yake Wapalestina takribani 8500 wanaishi katika eneo linalozungukwa kati ya uzio huo na msitari wa kijani unaotenganisha maeneo hayo.

Na Nabi Samwil uzio huo unatenganisha kijiji hicho na eneo lingine la Ukingo wa Magharibi na wakazi hawawezi kusafiri kwenda maeneo ya karibu ya Jerusalem bila vibali na kulazimika kupita katika vituo vya upekuzi kuingia vijiji vya jirani.

Katika baadhi ya shule alizotembelea Bi Amos amesema ameshuhudia madara mengine hayana hata madirisha na vifaa vichache hali ambayo haiwezi kurekebishwa kwa sababu mipango ya Israel hairuhusu na amesema hali hiyo haikubaliki.