Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban aitaka Hamas na Fatah kuzingatia mkataba wa amani

Ban aitaka Hamas na Fatah kuzingatia mkataba wa amani

Wakati makundi mawili hasimu ya Palestina Hamas na Fatah yametia saini makubaliano ya kumaliza tofauti zao na kuwa kitu kimoja hii leo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon wamewataka kuzingatia misingi ya kidiplomasia kumaliza mzozo wa Israel na Palestina.

Ban Ki-moon

Ban ameyataka makundi hayo yaliyosaini mkataba leo mjini Cairo Misri kujizatiti na kufuata mapendekezo ya Quartet ambayo yanataka suluhisho la kuwa na mataifa mawili yaani Palestina na Israel na kuishi pamoja kwa amani na usalama Mashariki ya Kati.

Wiki iliyopita wawakilishi wa Hamas na Fatah walitangaza kufikia muafaka chini ya upatanishi wa Misri, kuunda serikali ya umoja wa kitaifa na kufanya uchaguzi mkuu ndani ya mwaka mmoja. Hamas ambayo hailitambui taifa la Israel ilichukua udhibiti wa Gaza mwaka 2007 baada ya kukitoa madarakani chama cha Fatah cha Rais Mahmoud Abbas anayedhibiti eneo la Ukingo wa magharibi.

Mratibu maalumu wa Umoja wa mataifa kwa amani ya Mashariki ya Kati Robery Serry amekuwa Cairo kushuhudia utiaji saini wa leo.