Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Haki za nyumba ziko hatarini Barazili ikijiandaa na kombe la dunia

Haki za nyumba ziko hatarini Barazili ikijiandaa na kombe la dunia

Wakati Brazili ikijiandaa kuwa mwenyeji wa kombe la dunia la kandanda hapo 2014 na michuano ya Olimpiki 2016 kuna madai mengi yaliyojitokeza kuhusu ukiukwaji wa haki za nyumba.

Kwa mujibu wa mwakilishi wa baraza la haki za binadamu kuhusu haki za nyumba bora Raquel Rolnik amepata madai ya watu kutolewa kwa nguvu kwenye nyumba nakutokuwa na makazi, hali ambayo inaweza kusababisha ukiukaji wa haki za binadamu. Jason anayo taarifa zaidi.

(RIPOTI YA JASON NYAKUNDI)

Bi Rolnik amesema kuwa ameshangazwa na fidia ndogo zinazolipwa kwa jamii zilizoathirika ikilinganishwa na gharama ya maeneo hayo ambapo maandalizi ya mashindano ya kombe la dunia na ya Olimpiki yanapofanyika.

Amesema kuwa kuwalipa fidia kidogo waathiriwa huenda kukasababisha watu kukosa makao au kuibuka kwa makao mengine duni, familia nyingi zinaondolewa makwao kwa nguvu bila ya kupewa muda wa kutafuta njia mbadala huku maeneo wanakopelekwa yakiwa hayana miundo msingi .

Ametoa mfano mjini Rio de Janeiro ambapo familia nyingi huenda zikapoteza makwao ili kutoa nafasi kwa miradi inayohusiana na maandalizi ya kombe la dunia na mashindano ya Olimpiki mjini Sao Paulo ambapo pia familia nyingi zitahamishwa wakati mji huo unaporembeshwa.