Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Gbagbo na washirika wake kukumbwa na vikwazo vya baraza la usalama

Gbagbo na washirika wake kukumbwa na vikwazo vya baraza la usalama

Baraza la usalama leo limeamua kuidhinisha vikwazo vilivyoainishwa kwenye azimio namba 1572 la mwaka 2004 dhidi ya baadhi ya watu nchini Ivory Coast.

Vikwazo hivyo ni kwa wale wanaozuia amani na upatanisho nchini Ivory Coast, wanaozuia kazi za mpango wa Umoja wa Mataifa nchini humo UNOCI na wadau wengine wa kimataifa na pia wanaotekeleza ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu na sheria za kimataifa za masuala ya kibinadamu.

Vikwazo vitakavyowakabili wahusika ni pamoja na vya fedha na kusafiri na orodha ya watu hao kwa mujibu wa baraza la usalama ni Rais wa zamani wa Ivory Coast Laurent Gbabo ambaye ameelezwa kuwa kizingiti cha amani na upatanisho na pia kuyakataa matokeo ya uchaguzi mkuu wa Rais, mwenyekiti wa kundi la wabunge wa FPI Simone Gbagboambaye pia anashutumiwa kwa kuzuia amani, machakato wa upatanishi na kuchochea chuki na ghasia.

Wengine ni Desire Tagro katibu mkuu katika serikali ya Gbagbo ambaye anadaiwa kushiriki katika serikali haramu, kuzuia amani na mchakato wa maridhiano, kukataa matokeo ya uchaguzi na kushiriki katika ghasia.

Vikwazo pia vitamkubwa mwenyekiti wa chama cha FPI Passcal Affi N'Guessan kwa kuzia amani na mchakato wa maridhiano na kuchochea chuki na ghasia. Na wa mwisho ni Alcide Djedje mshauri wa karibu wa Laurent Gbagbo.