Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Operesheni za anga pekee hazitoshi kumaliza mzozo wa Libya:Ban

Operesheni za anga pekee hazitoshi kumaliza mzozo wa Libya:Ban

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon leo amehutubia mkutano wa kimataifa kuhusu Libya unaofanyika mjini London Uingereza.

Amewaambia viongozi kutoka nchi zaidi ya 35 wakiwemo mawaziri, maafisa wa NATO, Muungano wa Afrika na jumuiya ya nchi za Kiarabu waliokusanyika kwenye mkutano huo kwamba ingawa hatua za jumuiya ya kimataifa zimeokoa maisha ya maelfu ya watu , operesheni za anga pekee haziwezi kutatua mzozo wa Libya, wala kuleta suluhisho ambalo litakidhi matakwa ya watu wa Libya.

Ban amesema mwakilishi wake maalumu atarejea punde nchini Libya kukutana na pande zote, yaani viongozi wa serikali na wale wa upinzani.

(SAUTI YA BAN KI-MOON)

Ban ameongeza kwamba maendeleo na hatua za haraka nchini humo zinahitaji sote kutazama mbele na muda si mrefu watu wa Libya itabidi washirikiane. Amesema lengo la muda mrefu la Umoja wa Mataifa ni kuwasaidia watu wa Libya kufanikisha azma hiyo, kuwa na mipango ya mpito itakayowasaidia kuelekea kwenye demokrasia.