Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wanawake ni suluhu ya matatizo ya njaa:WFP

Wanawake ni suluhu ya matatizo ya njaa:WFP

Katibu mkuu wa shirika la mpango wa chakula duniani WFP Josette Sheeran amewataja akina mama kama kiungo muhimu katika kukabiliana na tatizo la njaa duniani.

Akiongea wakati wa maadhimisho ya siku ya kimataifa ya akina mama, Sheeran aliwataja akina mama kama Graça Machel, mama Teresa, Aung San Suu Kyi na wengine wengi kama mfano mzuri kwa mamilioni ya akina mama kote duniani ambao wanajitahidi kila siku kuwahakikishia maisha mema watoto wao.

Sheeran anasema kuwa njaa ndilo tatizo kubwa wakati huu ambapo takriban watu bilioni moja wanapokabiliwa na tatizo hilo akisema kuwa akina mama ndio kiungo muhimu cha kukabiliana nalo. Sheeran ametoa mfano wa Syria , Cameroon, Nepal ambapo takriban akina mama 342,000 walio kwenye uongozi wamepewa mafunzo juu ya masuala ya usambazaji wa chakula kama moja ya njia ya kuhakikisha kuwa watoto wamepata chakula.