Uchunguzi ufanyike kuhusu mashambulizi Afghanistan:Coomaraswamy
Mjumbe wa Umoja wa Mataifa anayehusika na watoto pamoja na maeneo yaliyokumbwa na mizozo ya vita,ametaka kuwepo kwa uchunguzi kufuatia vikosi vya jumuiya ya kujihami NATO kufanya shambulizi huko Kaskazini mwa Afghanistan na kuuwa watoto tisa.
Mjumbe huyo Radhika Coomaraswamy amesema kuuliwa kwa watoto hao ni jambo la kusikitisha na linatoa changamoto ambayo lazima itafutiwe ufumbuzi tena na mapema. Amesema ni lazima kuanzisha utaratibu wa kuangalia namna mashambulizi hayo yanavyoendeshwa ili kuwakinga wananchi na matukio kama hayo.
Kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari, watoto hao waliuwawa wakati wakiwa kwenye eneo moja wakisaka kuni. Kamanda wa vikosi hivyo vya NATO David Petraeus ameripotiwa akiomba radhi kutokana na tukio hilo.