UNHCR yahofia wakimbizi wanaovuka toka Libya
Idadi ya wakimbizi kutoka Libya wanaokimbia machafuko nchini mwao na kuelekea katika nchi ya jirani Tunisia imepungua na shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wakimbizi hao UNHCR limeonya kuwa hali hiyo siyo ishara njema kwa mustakabala wa wakimbizi hao.
Duru zinasema kuwa hadi sasa kumekuwa na idadi ndogo ya wakimbizi wanaovuka mpaka kuingia Tunisia wanaofika 2,000 kwa siku tofauti na ilivyokuwa hapo nyuma ambapo wakimbizi kati ya 10,000 hadi 15,000 walivuka mipaka kwa siku.
Ikizungumzia hali hiyo, UNHCR imesema kuwa kupungua kwa idadi hiyo kunaweza kusababishwa na hali mbaya ya usalama inayoendelea sasa nchini Libya na taarifa zaidi zinasema kuwa vikosi vya jeshi vimezingira eneo la mpakani kudhibiti kundi la wakimbizi kuhama nchini mwao.
Mashirika ya umoja wa mataifa yanaendesha juhudi za kuwanusuru wakimbizi hao ambao baadhi yao wamekosa wamasiliano kabisa.