Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Global Fund yataka dola milioni 34 zirejeshwe kutoka nchi 4

Global Fund yataka dola milioni 34 zirejeshwe kutoka nchi 4

Mfuko wa kimataifa Global Fund wa kupambana na ukimwi, kifua kikuu na malaria unadai kurejeshewa dola milioni 34 ambazo hadi sasa haziaelezewa zilivyotumika katika baadhi ya nchi.

Ripoti ya mkaguzi mkuu wa mfuko huo ya mwaka jana inaonyesha kwamba kulikuwa na matumizi mabaya ya fedha hizo katika nchi nne kati ya 145 zilizopokea msaada kupambana na maradhi hayo matatu. Mkuu wa Global Fund Michel Kazatchkine amewaambia waandishi wa habari mjini Geneva kwamba mfuko huo hauna subira kwa masuala ya ufisadi. Amesema

"Global Fund inataka kurejeshwa kwa dola milioni 34 ambazo hazijatolewa maehesabu yake kwa hizi na nchi zingine ambazo ni kati ya dola bilioni 13 zilizotolewa.Global Fund inashirikiana na nchi husika kuhakikisha kwamba wanaofanya ufisadi wanafikishwa kwenye sheria. Kesi za uhalifu tayari zimeanza nchini Mali, Mauritania na Zambia."

Global Fund ni mfuko wa ushirikiano binafsi na umma ambao unahusika na kuchangisha fedha na kuzigawa kwa ajili ya kuzuia na kutibu ukimwi, kifua kikuu na malaria.