Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ujenzi wa makazi ya walowezi wa Israel usitishwe:Pascoe

Ujenzi wa makazi ya walowezi wa Israel usitishwe:Pascoe

Israel imetakiwa kwa mara nyingine na mkuu wa masuala ya kisiasa wa Umoja wa Mataifa kusitisha ujenzi wa makazi ya walowezi katika maeneo yanayokaliwa ya wapalestina.

Lynn Pascoe, ameliambia baraza la usalama la Umoja wa Mataifa hii leo kwamba majadiliano ya amani baina ya Israel na Palestina bado yako njia panda. Ameonya kuwa ujenzi zaidi wa makazi ya walowezi kwenye Ukingo wa Magharibi ikiwemo Jerusalemu unaendelea kuwa kikwazo cha majadiliano ya amani na suluhisho la kudumua la masuala ya Mashariki ya Kati.

Masuala hayo ni pamoja na mipaka, udhibiti wa Jerusalemu, makazi ya Walowezi, haki ya maji na hadhi ya kisheria ya wakimbizi wa Palestina, kwa kufuata njia ya amani ya eneo hilo. Njia ya amani ya Mashariki ya Kati kumaliza mgogoro baina ya Israel na Wapalestina ilipendekezwa na kundi la pande nne Quartet linalojumuisha Umoja wa Mataifa, muungano wa Ulaya, Marekani na Urusi.