Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Somalia yaimarisha ulinzi kwa msaada wa Japan na UM

Somalia yaimarisha ulinzi kwa msaada wa Japan na UM

Mwaskilishi maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia, Augustine P. Mahiga, leo ameishukuru serikali ya Japan, washirika wa Umoja wa Mataifa na mashirika ya kikanda kwa msaada wao kwa serikali ya mpito ya Somalia.

Mahiga ametoa shukrani hizo wakati wa sherehe za kuapishwa polisi 500 walioamaliza mafunzo. Rais wa Somalia Sheikh Sharif Sheikh Ahmed na Rais wa Djibouti, wamehudhuria pia hafla hiyo iliyofanyika katika chuo cha mafunzo ya polisi cha Djibouti.

Kurejesha na kudumisha usalama ni moja ya vipengee muhimu vilivyoko kwenye mkataba wa amani wa Djibouti na pia ni moja ya masuala yanayopewa kipaumbele na serikali ya mpito ya Somalia kwa ajili ya kuhakikisha utulivu, kuleta maridhiano ya kisiasa, kusaidia ujenzi mpya, na kuwezesha ujenzi mpya wa kuleta maendeleo endelevu amesema balozi Mahiga.

Mahiga ameipongeza serikali ya Djibouti kwa msaada na ushirikiano wake na UNIPOS na kusema ni mfano wa kuigwa na wengine katika kanda, kwa kutoa mazingira mazuri ya kuwezesha mkataba wa Djibouti kuweza kutekelezwa .

Pia ametoa shukrani zake kwa serikali ya Japan kwa mchango wake wa dola milioni 10 kwa mfuko wa UNIPOS kwa ajili ya kusaidia sekta ya ulinzi, taasisi za usalama ambapo amesema bila fedha hizo isingewezekana kutoa mafunzo.

Mbali ya mafunzo msaada huo unasaidia kupata vifaa kama magari ya polii, vifaa vya mawasiliano na kuboresha miundombinu mjini Moghadishu.