Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Waandishi habari wanaofanya kazi kwenye maeneo ya vita walindwe: UNESCO

Waandishi habari wanaofanya kazi kwenye maeneo ya vita walindwe: UNESCO

Shirika la Umoja wa Mataifa la elimu, sayansi na utamaduni UNESCO ambalo pia linapigania uhuru wa habari na wa kujieleza leo limetoa wito wa kuimarisha usalama kwa waandishi na wafanyakazi wengine wa sekta ya habari wanaofanya kazi kwenye maeneo ya vita au machafuko ya kijamii.

Wito huo unafuatia kuchapishwa wiki jana mtazamo wa hali ya waandishi wa habari kwa mwaka huu 2010 ambapo imebainika kwamba waandishi habari 42 wameuawa mwaka huu pekee.

Kwa mujibu wa Irina Bokova mkurugenzi mkuu wa UNESCO idadi ya waandishi wa habari waliouawa mwaka huu japo ni ndogo ikilinganishwa na mwaka jana lakini ni jambo lisilikubalika, na inadhihirisha mazingira magumu ya kazi yanayowakabili waandishi wa habari.

Amesema mashambulio ya kujitoa muhanga na ghasia mitaani zimechangia vifo vingi na amezitaja nchi zinazoongoza kwa mauaji ya waandishi habari ni Pakistan ambako 8 wameuawa, Iraq wane, Honduras watatu na Mexico watatu.