Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UM waitaka Myanmar kuharakisha maendeleo ya demokrasia

UM waitaka Myanmar kuharakisha maendeleo ya demokrasia

Mjumbe wa Umoja wa mataifa ailiyeko ziarani nchini Myanmar amezihimiza mamlaka nchini humo kuweka nguvu zaidi kwenye ujenzi mpya wa demokrasia na maridhiano ya kitaifa hasa katika kipindi hiki ambacho taifa hilo linaanza safari mpya.

Vijay Nambiar, ambaye ni mwakilishi wa Katibu Mkuu nchini humo amesema kuwa huu ni wakati kwa viongozi kuanza kushughulikia kero na mashaka yaliyoibuka wakati wa uchaguzi mkuu uliopita. Mjumbe huyo amesema kuwa amekutana na pande mbalimbali ambako amepokea kilio kinachoelezea wasiwasi walionao wananchi kuhusiana na namna mchakato wa uchaguzi mkuu ulivyoendeshwa, hivyo amezitaka mamlaka zinazohusika kushughulikia kasoro zote zilizojitokeza.

Nchi hiyo ilifanya uchaguzi wake wa kwanza katika kipindi cha miaka 20 iliyopita November 7, uchaguzi ambao uliangaliwa kama kipimo cha kuanza kuchipua upya kwa demokrasia iliyokandamizwa kwa miaka mingi.