Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkuu wa haki za binadamu wa UM kuzuru nchini Bolivia

Mkuu wa haki za binadamu wa UM kuzuru nchini Bolivia

Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Navi Pillay atazuru Bolivia kuanzia ovember 12 hadi 16 mwaka huu ambako atakutana na Rais Evo Morales Ayma.

Nia ya ziara ya Bi Pillay ni kupata uelewa wa hali halisi ya jimbo la Plurinational la nchi hiyo hasa kuhusiana na haki za binadamu, ikiwa ni pamoja na hatua zilizopigwa katika baadhi ya nyanja na masuala yaliyo na utata. Katika ziara yake hiyo pia ataangalia njia muafaka ambazo zitatumiwa na ofisi yake kutoa msaada na ushauri kwa serikali ya Bolivia. Jayson Nyakundi na taarifa kamili

(RIPOTI YA JAYSON NYAKUNDI)

Ziara ya bi Pillay inafanyika baada ya maafikiano ya hivi majuzi na serikali ya Bolivia yanayoruhusu kuongezwa muda wa kuwepo kwa ofisi za tume ya kutetea haki za binadamu nchini Bolivia hadi mwaka 2013.  Ofisi hiyo ilibuniwa mwaka 2007 kutoa usaidizi wa kiufundi kwa mashirika ya kiserikali na yale ya umma, kuhakikisha kuwepo kwa haki za binadamu na pia kuchunguza na kutoa ripoti kuhusu hali ya haki za binadamu nchini Bolivia. 

Kando na kutana na rais Evo Morales, afisa huyo pia atakutana na mawaziri akiwemo waziri wa mambo ya kigeni, waziri wa sheria, maafisa wa ngazi za juu serikalini pamoja na waakilishi wa bunge na mahakama.