Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Wanajeshi zaidi kupelekwa Ivory Coast:UM

Wanajeshi zaidi kupelekwa Ivory Coast:UM

Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa limevishauri vyama vya siasa nchini Ivory Coast kuhakikisha kuwa uchaguzi wa Urais ambao umekuwa ukiahirishwa kufanyika kwa mani na utulivu.

Uchaguzi huo sasa umepangwa kufanyika mwezi ujao baada ya ule wa awali wa 2005 kutofanyika kutokana na machafuko ya kisiasa. Baraza hilo ambalo limekuwa likitathimini hali ya Ivory Coast pia limepitisha azimio la kuongeza wanajeshi 500 zaidi kulinda usalama wakati wa uchaguzi. Jayson Nyakundi anayo taarifa zaidi.

(RIPOTI YA JASON NYAKUNDI)

Kupitia kwa ripoti iliyotolewa kwa vyombo vya habari na balozi Ertugrul Apakan kutoka nchin Uturuki, nchi ambayo ni rais wa baraza la usalama la umoja wa Mataifa mwezi huu amesema kuwa washikadau wote kwenye uchaguzi huo wanastahili kuhakikisha kuwa awamu ya kwanza ya uchagzuzi nchini Ivory Coast itafanyika tarehe 31 mwezi Oktoba mwaka huu.

Wanachama hao 15 wa baraza la usalama la UM wamevitaka vyama kuhakikisha kuwepo kwa amani kabla , wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi. Ujumbe wa UM nchini Ivory Coast unaofahamika kama UNOCI umekuwa ukitoa usaidizi wa kiufundi kwa maandalizi ya uchaguzi wa urais ambao ulistahili kuandaliwa tangu mwaka 2005 baada ya nchi hiyo kuvurugwa na vita mwaka 2002 na kugawanyika mara mbili kati ya eneo la kaskazini linalodhibitiwa na waasi na lile la kusini lililo chini ya serikali.