Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Mkuu wa MONUSCO ahofia machafuko Kivu Kaskazini DR Congo

Mkuu wa MONUSCO ahofia machafuko Kivu Kaskazini DR Congo

Mkuu wa mpango wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo MONUSCO, leo ameelezea hofu yake juu ya kuendelea kwa mapigano katika jimbo la Kivu ya Kaskazini ambako serikali inachunguza mauaji ya hivi karibuni.

Mkuu huyo Roger Meece ambaye pia ni mwakilishi maalumu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo amesema anaunga mkono nia ya serikali kuchunguza ghasia hizo na kuwafikisha wahusika kwenye vyombo vya sheria. Uwepo wa makundi mbalimbali ya wanamgambo yamesababisha machafuko kwenye jimbo la Kivu ya Kaskazini katika muongo mzima uliopita, ukosefu wa usalama na kuwafungisha virago maelfu ya watu.

Wafanyakazi wa misaada wa Umoja wa Mataifa hivi karibuni wamekadiria kwamba watu takribani 890,000 wamekuwa wakimbizi wa ndani. Mwishoni mwa mwezi Julai na mwanzoni mwa Agost mwaka huu makundi yenye silaha yaliwabaka mamia ya watu Kivu ya Kaskazini wakiwemo watoto zaidi ya 20.