Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

UNHCR na DR Congo wameanza ugawaji wa vitambulisho wa wakimbizi

UNHCR na DR Congo wameanza ugawaji wa vitambulisho wa wakimbizi

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR na serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo leo wameanza ugawaji wa vitambulisho kwa wakimbizi walioko nchini humo.

Vitambulisho hivyo ambavyo vinagawiwa kwa wakimbizi 173,000 vina lengo la kuimarisha haki za wakimbizi hao kwani vitambulisho ni sawa na vibali vya kuishi nchini humo, na kuwa na haki kama raia wa Congo kwa mujibu wa sheria za wakimbizi zilizopitishwa Congo Oktoba 2002.

UNHCR inasema miongoni mwa haki hizo ni kuweza kufanya kazi, kusoma, kupata huduma za afya na kuwa huru kuhama sehemu moja hadi nyingine ndani ya nchi hiyo. Kundi la kwanza la wakimbizi 3300 wanapewa vitambulisho vyao katika mji mkuu Kinshasa na kisha vitagawiwa katika majimbo yote nchini humo kwa wakimbizi hao ambao wengi ni kutoka Angola, Rwanda na Burundi.