Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Ban na waziri wa Serbia wajadili suala la Kosovo na upokonyaji silaha

Ban na waziri wa Serbia wajadili suala la Kosovo na upokonyaji silaha

Masuala yanayohusu Kosovo na mkutano wa ngazi za juu wa upokonyaji silaha wa Septemba ndizo zimekuwa ajenda kuu leo kwenye mkutano wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon na waziri wa mambo ya nje wa Jamhuri ya Serbia Vuk Jeremic.

Taarifa ya ofisi ya msemaji wa Umoja wa Mataifa kuhusu mkutano huo inasema kuhusu Kosovo Katibu mkuu amesema ana panga kuratibu hatua inayofuata na muungano wa Ulaya, ambao umejitolea kusimamia mchakato wa majadiliano baina ya Pristina na Belgrade.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa Katibu mkuu pia amejadili mswada wa Serbia kwa baraza kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu mada hiyo. Ban ameendelea kuziomba pande zote kuunga mkono mazungumzo na kumaliza matatizo yote yaliyosalia na kuepuka purukushani.

Wiki jana mahakama ya juu ya Umoja wa Mataifa ICJ mjini The Hague iliamua kwamba uamuzi wa Kosovo wa kujitenga na Serbia mwaka 2008 haukukiuka sheria za kimataifa.